Ruka hadi kwenye maudhui makuu

SABATO.

Maana ya neno sabato.
Sabato ni neno linalotokana na neno la Kiebrania “Shabbat” ambalo lina maana  kuacha, au kupunzika (kustarehe). Kutokana na utaratibu wa Mungu kulikuwa na Sabato mbili.

Sabato ya kwanza.
Mungu aliumba vitu vyote kwa siku sita. Siku ya saba aliacha kufanya kazi akapumzika. Hii ni sabato kwa ajili Mungu. “Basi mbingu na nchi zikamalizika, na jeshi lake lote. Na siku ya saba alimaliza kazi yake yote aliyoifanya; akastarehe siku ya saba ,akaacha kufanya kazi yake yote aliyoifanya. Mungu akaibarikia siku ya saba, akaitakasa kwa sababu siku hiyo Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya…” Mwanzo 2:1- 4.

Sabato ya pili.
Hii ilikuwa ni sabato kwa ajili ya wana wa Israeli. Mungu alipowatoa wana wa Israeli utumwani Misri, kwa kumtumia mtumishi wake Musa, aliwapa amri ya sabato. Sababu ya kupewa sabato ni ili wamkumbuke  Mungu  aliwaokoa kutoka utumwani Misri. “Nawe utakumbuka ya kuwa wewe ulikuwa utumwani katika nchi ya misri, na yakuwa Bwana, Mungu wako, alikutoa huko kwa mkono wenye nguvu, na mkono ulionyoshwa; kwa sababu hiyo Bwana,Mungu wako, alikuamuru uishike sabato.” Kumbukumbu 5:15.  Katika sabato hii Mungu  alifanya iwe ishara kati yake na Israeli.

Maana ya neno ishara.
Neno ishara linatokana na neno la Kiebrania  “ot” ambalo linamanisha (a) Ishara, alama; (b) Ishara ya ajabu, muujiza. Mungu aliifanya iwe ni ishara kati yake na wana wa Israeli, kwa sababu baada ya uumbaji alipumzika kufanya kazi; Imeandikwa:  “Ni ishara kati ya   mimi na wana Israeli milele; kwani kwa siku sita Bwana alifanya  mbingu na nchi, akastarehe siku ya saba na kupumzika.” Kutoka 31:17. Mungu aliwaagiza wana wa Israeli  kuitunza sabato.                               
Maana ya kuitunza sabato.
Siku ya saba wana Israeli walipaswa kuzingatia kama ifuatavyo: Kuacha kufanya kazi yoyote na ikiwa mtu aliivunja amri hii aliuawa. Mungu aliwapa agizo kwa kusema,  “Kazi itafanywa siku sita; lakini siku ya saba ni sabato ya kustarehe kabisa, takatifu kwa Bwana; kila mtu atakayefanya kazi yoyote katika siku ya sabato, hakika yake atauawa.” Kutoka 31:15.

Wasiwashe  moto.
Wasingepika chakula siku ya saba ambayo ni sabato. “Hamtawasha moto katika nyumba zenu kwa siku  ya sabato.” Kutoka 35:3. 

Kuhani kuteketeza sadaka.
Kuhani alikuwa na ruhusa ya Mungu kufanya kazi ya kuteketeza sadaka. “Tena siku ya sabato watasongezwa  wana-kondoo wawili, waume wa mwaka wa kwanza,wakamilifu pamoja na sehemu kumi mbili za efa za unga mwembaba kuwa sadaka ya unga,  uliochanganywa na mafuta, pamoja na sadaka yake ya kinywaji; hii ndiyo sadaka ya kuteketezwa kila sabato...”  Hesabu 28:9,10.

Sabato wakati wa Agano Jipya.
Agano Jipya ni kipindi kinachoelezea habari za  kuzaliwa, kufa, kufufuka na kupaa kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Katika kipindi hiki hata sasa sheria ya  zamani ya Musa kuhusu sabato ilibatilishwa na kufanywa upya. Ndiyo maana  Yesu alimponya mtu siku ya sabato, akasema “ …Basi ni halali kutenda mema siku ya sabato” Mathayo 12:12. Alikuwa na mamlaka ya kufanya lilo njema siku ya sabato. Yeye ndiye  aliifanya sabato;  kwa kuwa imeandikwa: “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakukufanyika chochote kilichofanyika.” Yohana 1:3.

Baada ya Yesu  kumpomya mtu siku ya sabato, viongozi wa dini na sheria ya Mungu wakaona na kufikiri ameivunja sabato. Lakini kwa kutokuyafahamu maandiko hawakumjua Yesu ni nani. Yesu alikuwa ni Bwana wa sabato na ni kuhani milele,  Yesu akawaambia; “Wala hamkusoma katika torati, siku ya sabato makuhani hekaluni huinajisi sabato wasipate hatia? Kwa maana mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.  Kisha akamwambia yule mtu, nyosha mkono wako; akaunyosha , ukapona, ukawa mzima kama wa pili.” Mathayo 12:3,8,13. 

  Je, wakati wa agano jipya tunatunza sabato?
Katika torati (sheria) iliandikwa mambo mengi ambayo iliamuru yafuatwe, ambayo yalikuwa ni kivuli cha agano jipya; ndiyo maana imeandikwa: “Basi, mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.”  Wakolosai 2:16,17. Katika haya maandiko, Wakolosai wanashauriwa ya kwamba mtu asiwahukumu kwa kutokuifuata torati kuhusu vyakula, vinywaji, sikukuu,  mwandamo wa mwezi na sabato.

“Basi, sasa mkiisha kumjua Mungu, au zaidi kujulikana na Mungu, kwa nini kuyarejea mafundisho ya kwanza “torati” yaliyo manyonge, yenye upunguvu, ambayo mnataka kuyatumikia tena? Mnashika siku, na miezi, na nyakati, na miaka.” Wagalatia 4:9,10. Maandiko haya yaliwaonya  Wagalatia waache mafundisho waliyoyarudia  na kuyatumikia, kwa sababu ni manyonge, yana upunguvu, yasingewakamilisha katika neno la Mungu. “Maana, kuna kubatiliwa ile amri iliyotangulia, kwa sababu ya udhaifu wake, na kutokufaa kwake; (kwa maana ile sheria haikukamilisha neno); …….”  Waebrania 7:18,19. 

Sabato kukoma.
Yesu aliponya mara kwa mara siku ya sabato, kwa sababu hiyo isingetunzwa tena. Wakati wa sabato ulikuwa karibu kwisha kwa sababu amekuja Bwana wa sabato kuikamilisha sheria. Isingalikuwako tena, ilibatilishwa,  ndiyo maana Yesu alifanya kazi siku ya sabato,  akawajibu Wayahudi akasema.  “……Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi.” Yohana 5:10,17.  Ndiyo maana sasa yatupasa:

Kumwabudu Mungu katika roho.
“Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu “Hekaluni”. Lakini saa inakuja, na sasa ipo, ambao waabuduo halisi watamwabudu Baba katika Roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, na wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika Roho na kweli.” Yohana Yn 4:21,23-24.  Kwa    sababu hiyo tunahesabiwa haki.

Kuhesabiwa haki kwa imani.
Hivi sasa ni wakati wa agano jipya, ambalo lilifanyika kwa damu ya Yesu Kristo iliyomwagika msalabani. Agano hili ni bora kuliko lile la zamani kwa sababu kila amwaminiye anahesabiwa haki bure. Sii kwa kutenda kwa matendo ya sheria kama kutunza sabato, kutoa sadaka za dhambi na matendo mengine ambayo sheria iliagiza. “Kwa maana Kristo ni mwisho wa sheria, ili kila amwaminiye ahesabiwe haki.”  "Lakini sasa haki ya Mungu imedhihirishwa paspo sheria; inashuhudiwa na torati na manabii; ni haki ya Mungu iliyo kwa njia ya imani katika Kristo Yesu kwa wote wamwaminio. Maana hakuna tofauti;” Warumi 3:21;10:4. Imewekwa wazi ya kwamba haki inapatikana kwa imani ilishuhudiwa na torati na manabii, huu ni ushahidi  wa kutosha. Neno lolote huthibitika kwa vinywa vya mashahidi zaidi ya mmoja. "... Kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike". Mathayo 18:16.

Maoni

  1. Bila jina23:17

    Umeeleweka saana Mungu akubariki 5

    JibuFuta
  2. Bila jina08:28

    Bwana Mungu awabariki kwa mafundisho yenu yenye kutukuza kiroho, AMINA.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

KUMTUMIKIA MUNGU KWA BIDII.

Kutokana na kichwa cha somo hapa juu katika matukio wazi ili mtu amtumikie Mungu ni lazima awe na bidii. Kwa sababu hiyo kwa mtu yule ambaye ameweka nia moyoni mwake ya kwamba atatumikia Mungu kwa bidii. Tukiangalia kuhusu mwanadamu kuna mambo mengi katika maisha yake ameyafanya kutokana na bidii aliyo nayo. Lakini ikiwa mtu hana bidii kwa ajili ya mambo ya Mungu kamwe hawezi kuingia ufalme wa Mungu. Ndio maana imeandikwa;  "Tangu siku za Yohana Mbatizaji hata sasa ufalme wa mbinguni hupatimkana kwa nguvu, nao wenye nguvu wauteka,   Mathayo 11:12 ."    " Torati na manabii vilikuwapo mpaka Yohana; tangu wakati huo habari njema ya ufalme wa Mungu hutangazwa, na kila mtu hujiingiza kwa nguvu."   Luka 16:16. Hapa ninatoa ushuhuda wangu binafsi, kuhusu kumtumikia Mungu kwa bidii. Wakati nilipookoka nilikuwa na kiu au shauku kwa ajili ya kutaka kujazwa Roho Mtakatifu. Kwa sababu nilikuwa ninamhitaji sana nilimwomba mtumishi mmoja wa Mungu aniombee ili niweze kujazwa...

KUISHI MAISHA YA UTAKATIFU.

Utakatifu  - Ni maisha ya Mkristo anayoyaishi kwa kuzingatia kanuni ya neno la Mungu baada ya kumkiri na kumpokea Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yake. Kuishi maisha ya utakatifu ni jambo linalowezekana, kwa sababu Mungu alipomuumba mwanadamu alimwekea hiari ndani yake kwa kutokea kwa tukio. Ndio maana Yesu alipokuwa akifundisha alitumia mfano wa mti kuonyesha mtu anavyoweza kuishi maisha haya ya kumpendeza Mungu au ya maisha ya dhambi. "   "Ufanye mti kuwa mzuri na matunda yake kuwa mazuri, au ufanye mti kuwa mbaya na matunda yake mabaya, kwa maana kwa matunda yake mti hutambulikana" Mathayo 12:33. Kuishi maisha ya utakatifu ni agizo la Mungu kwa wale wote aliowachagua. Ndio maana Mungu alimwambia Musa,   "Nena na makutano wote na wana wa Israel, uwaambie, mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi Bwana Mungu wenu ni mtakatifu"  Walawi    19:2. Kuwa mtakatifu ni kumpendeza Mungu, kwa sababu amesema;  “Watakatifu waliopo duniani ndio walio bora...

TUNDA LA UAMINIFU.

Uaminifu ni mojawapo ya tunda la Roho katika maandiko matakatifu. Tutajifunza uaminifu wa Mungu unaopatikana katika neno lake. Yeye amesema atatimiza yale aliyoahidi katika neno lake, si tu kwa wana wa Israel bali kwa watu    wote wanaoishi sawasawa na neno lake. Kwa hiyo, kwa upande wetu inatupasa sisi nasi kuwa waaminifu kwa kuliishi na kulitenda neno la Mungu.   “Basi jueni ya kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake, hata vizazi elfu.   Na itakuwa, kwa sababu mwazisikiza hukumu hizi, na kuzishika na kuzitenda, basi Bwana, Mungu wako, atakutimizia agano na rehema aliyowaapia baba zako.”   Kum 7:9, 12.   “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu    halitanirudia bure bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.   Isa 55:11" Tabia ya mtu mwaminifu. 1. Mtu aliye mwaminifu ni yule ambaye anatenda sawa...