Ruka hadi kwenye maudhui makuu

IMANI KAMILI KWA MTU ALIYEOKOKA.

Mkristo ambaye  ameokoka anapaswa kuwa na imani iliyo kamili. Mtu huyo anaweza kuwa na imani kamili iwapo  atazingatia na kuzitenda sheria zote za Mungu. Jambo hili ni la muhimu kwa kila mtu anayetarajia kuurithi ufalme wa Mungu. Iwapo mtu  atakuwa anatenda baadhi ya sheria za Mungu na kuziacha nyingine huyo atakuwa amefanya au kuenenda  kinyume na imani ya neno la Mungu. Kwa maana hiyo mtu wa namna hiyo hataweza  kuurithi ufalme wa Mungu.Yafuatayo ni mwendelezo wa  mambo  muhimu ya kuzingatia na kuyafanya ili mtu aweze  kuwa  na  imani iliyo kamili mbele za Mungu;
1. Kudumu katika  kutenda sawasawa na neno la Mungu.

2. Kila jambo lolote  unalolitenda ni lazima kuhakikisha liko  sawasawa na neno la Mungu.
3. Kudumu katika kuomba kila siku.
Mtu anayezingatia kuomba humshinda yule adui na hila zake zote.  Jambo hili ni muhimu tunaweza kujifunza kutoka kwa  Bwana wetu Yesu Kristo na  mitume wake walivyoomba kwa bidii kila siku.  Wao ni kielelezo kwetu kwa sababu walidumu katika kuomba na pia waliweza kumshinda shetani na majaribu yake yote.

Kama mtu hazingatii kumwomba Mungu kila siku inakuwa ni mwanzo wa yeye kuanza kupoteza uhusiano wake na Mungu. Mtu wa namna hiyo hawezi kusimama imara na kuishi sawasawa na neno la Mungu linavyosema. Kwa sababu hiyo ni rahisi kutenda dhambi anapojaribiwa na yule mwovu. Ndio maana  Yesu aliwaagiza wale wanafunzi na kuwaambia;
 "Kesheni mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu". Mathayo 26:41.

4Kuutawala moyo wako na usiruhusu mawazo mabaya. Hili ni jambo  linalowezekana iwapo utaamua na kuweka nia ya kwamba hutawaza mawazo mabaya.

5. Kutawala kinywa  chako usinene maovu, maneno yasiyofaa, maneno ya hovyo ya mitaani na  ya utani (mzaha/masihara). Ikiwa mtu atasemezana  na mtu mwingine kwa utani kwa kufanya hivyo  atakuwa amesema uongo.

6. Kuzungumza kwa kiasi.
Usiwe mwepesi kuongea kupita kiasi kwa sababu kwa kufanya hivyo unaweza kumkosea Mungu. Ni jambo la  muhimu kufahamu ya kwamba kabla ya kusema au kujibu  neno lolote, yakupasa kwanza kufikiria  ili uweze kujua jinsi  ikupasavyo  kusema. Hapa ninasema hivyo kwa sababu katika kunena kuna mtego wa  kujikwaa. Dhambi ya namna hii  baadhi ya watu wengi  wanaifanya. Dhambi nyingine ambayo watu  wengi  wanaifanya  ni kusema uongo kwa kusudi  la kuficha mambo fulani ambayo hawataki yafahamike kwa watu wengine.

7. Kuutawala mwili wako na kujilinda ili usije ukafanya dhambi ya  uzinzi na uasherati. Jambo hii linawezekana ikiwa mtu  ataepuka kuangalia picha za watu wanaokutana kimwili katika mitandao. Ni muhimu pia kuepuka kusikiliza au kusoma habari za mambo machafu yanayohusu zinaa. 

8. Ni muhimu kujihadhari na kuepuka watu wanaowasema  wengine vibaya. Kwa kufanya  hivyo utakuwa umejilinda na kuepuka kusengenya watu wengine. Na pia unakuwa umeepuka kusikiliza maneno ya usengenyaji. Kwa sababu hiyo utakuwa umeepuka kushiriki dhambi za wengine. "...wala usizishiriki dhambi za watu wengine". 1Timohteo 5:22. 

9. Kuilinda imani yako. Unaweza kuilinda imani yako  kwa kuyakataa mafundisho ya uongo. Kamwe usikubali  kuyafuata kwa sababu kwa kufanya hivyo hautaurithi ufalme wa Mungu. Kwa  mwamini aliyeokoka ili aweze kufahamu mafundisho yaliyo ya kweli, na ni yapi yaliyo ya uongo,  ni muhimu  kujifunza neno la Mungu kwa bidii na kulifahamu.

10.Kuishi maisha ya utakatifu.
 Ni  jambo la muhimu sana kwa kila mtu ambaye ameokoka kufahamu ya kwamba ni  lazima kuwa na utakatifu kama Mungu alivyo mtakatifu. Maana yake ni kuishi maisha ya kumpendeza Mungu na kudumu katika dhamiri safi. Mtu wa namna hiyo ni yule anayejilinda na kuepuka dhambi."Palikuwa na mtu katika nchi ya Usi, jina lake alikuwa akiitwa Ayubu; mtu huyo aliku mkamilifu na uelekevu , ni mmoja aliyemcha Mungu, na kuepukana na uovu." Ayubu 1:1. "Twajua kuwa kila aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi; bali yeye aliyezaliwa na Mungu hujilinda, na wala yule mwavu hamgusi". 1Yohana 5:18. Kutokana na andiko hilo linaonyesha wazi ya kwamba mtu ambaye amezaliwa (aliyeokoka) haiwezekani akafanya dhambi ikiwa amejilinda  na kuepukana na dhambi.  Ikiwa mtu yeyote akisema hakuna anayeweza kuwa mtakatifu kama  Mungu au Yesu, huyo anapotea hayajui  maandiko ya neno la Mungu kwa ukamilifu. Maandiko yanashuhudia  ya kwamba mtu anaweza kuwa mtakatifu ikiwa anazitii sheria zote za Mungu. Tunapoangalia kwenye Biblia  katika Agano la kale na Jipya,  maandiko yamethibitisha ya kwamba walikuwepo watakatifu. Kwa sababu hiyo hata sasa  duniani wapo watakatifu ndio maana Mungu amesema; "Watakatifu waliopo duniani Ndio walio bora, Hao ndio niliopendezwa nao".  Zaburi 16:3.

11. Kuacha dhambi.
Ni muhimu kila mwamini aliyeokoka kufahamu ya kwamba ni jambo la lazima kuacha kutenda dhambi. Ndio maana imeandikwa "Ikiwa mtu amekufa kwa mambo ya dhambi” na neno lingine linasema “usitende dhambi tena".

A. Kuhusu mtu kufa, hapa nitaelezea mambo yanayohusu dhambi.  Ikiwa mkristo aliyeokoka anampenda Mungu na kuishi neno la Mungu linavyosema anakuwa amekufa kwa mambo ya dhambi. Dhambi haiwezi kumtawala tena, na wala haina  nafasi katika maisha yake. "...Tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki…"  1Petro 2:24.

B. Neno "Usitende dhambi tena" linamkataza mtu asirudie kutenda dhambi. Kwa maneno mengine linamaanisha kuwa kamwe usitende dhambi na pia kuziacha kabisa. "... Usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lilo baya zaidi". Yohana 5:14.

 12.Usiipende dunia na mambo yake na huku unamtumikia Mungu.
Hapa ninamaanisha ya kwamba mambo yale yote ambayo ni kinyume na neno la Mungu ujitenge nayo na kuyaacha kabisa. Ni  jambo la muhimu kujihadhari na kuepuka kuishi maisha ya uvuguvugu katika kumtumikia Mungu kwa sababu utakataliwa. Ikiwa mwamini anayo bidii katika mambo ya Mungu na huku  anaendelea na dhambi  huyo ni vuguvugu. Mtu wa namna hiyo siku ile ya mwisho atahukumiwa na kutupwa katika ziwa la moto ambalo ni Jehanum. Huko atakuwa anateseka mchana na usiku yaani wakati wote, milele na milele. "Nayajua matendo yako, hu baridi wala moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto.   Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu"  Ufunuo 3:15-16; "Na moshi wa maumivu yao hupanda juu hata milele na milele, wala hawana raha mchana wala usiku…" Ufunuo 14:11.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

KUMTUMIKIA MUNGU KWA BIDII.

Kutokana na kichwa cha somo hapa juu katika matukio wazi ili mtu amtumikie Mungu ni lazima awe na bidii. Kwa sababu hiyo kwa mtu yule ambaye ameweka nia moyoni mwake ya kwamba atatumikia Mungu kwa bidii. Tukiangalia kuhusu mwanadamu kuna mambo mengi katika maisha yake ameyafanya kutokana na bidii aliyo nayo. Lakini ikiwa mtu hana bidii kwa ajili ya mambo ya Mungu kamwe hawezi kuingia ufalme wa Mungu. Ndio maana imeandikwa;  "Tangu siku za Yohana Mbatizaji hata sasa ufalme wa mbinguni hupatimkana kwa nguvu, nao wenye nguvu wauteka,   Mathayo 11:12 ."    " Torati na manabii vilikuwapo mpaka Yohana; tangu wakati huo habari njema ya ufalme wa Mungu hutangazwa, na kila mtu hujiingiza kwa nguvu."   Luka 16:16. Hapa ninatoa ushuhuda wangu binafsi, kuhusu kumtumikia Mungu kwa bidii. Wakati nilipookoka nilikuwa na kiu au shauku kwa ajili ya kutaka kujazwa Roho Mtakatifu. Kwa sababu nilikuwa ninamhitaji sana nilimwomba mtumishi mmoja wa Mungu aniombee ili niweze kujazwa...

KUISHI MAISHA YA UTAKATIFU.

Utakatifu  - Ni maisha ya Mkristo anayoyaishi kwa kuzingatia kanuni ya neno la Mungu baada ya kumkiri na kumpokea Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yake. Kuishi maisha ya utakatifu ni jambo linalowezekana, kwa sababu Mungu alipomuumba mwanadamu alimwekea hiari ndani yake kwa kutokea kwa tukio. Ndio maana Yesu alipokuwa akifundisha alitumia mfano wa mti kuonyesha mtu anavyoweza kuishi maisha haya ya kumpendeza Mungu au ya maisha ya dhambi. "   "Ufanye mti kuwa mzuri na matunda yake kuwa mazuri, au ufanye mti kuwa mbaya na matunda yake mabaya, kwa maana kwa matunda yake mti hutambulikana" Mathayo 12:33. Kuishi maisha ya utakatifu ni agizo la Mungu kwa wale wote aliowachagua. Ndio maana Mungu alimwambia Musa,   "Nena na makutano wote na wana wa Israel, uwaambie, mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi Bwana Mungu wenu ni mtakatifu"  Walawi    19:2. Kuwa mtakatifu ni kumpendeza Mungu, kwa sababu amesema;  “Watakatifu waliopo duniani ndio walio bora...

TUNDA LA UAMINIFU.

Uaminifu ni mojawapo ya tunda la Roho katika maandiko matakatifu. Tutajifunza uaminifu wa Mungu unaopatikana katika neno lake. Yeye amesema atatimiza yale aliyoahidi katika neno lake, si tu kwa wana wa Israel bali kwa watu    wote wanaoishi sawasawa na neno lake. Kwa hiyo, kwa upande wetu inatupasa sisi nasi kuwa waaminifu kwa kuliishi na kulitenda neno la Mungu.   “Basi jueni ya kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake, hata vizazi elfu.   Na itakuwa, kwa sababu mwazisikiza hukumu hizi, na kuzishika na kuzitenda, basi Bwana, Mungu wako, atakutimizia agano na rehema aliyowaapia baba zako.”   Kum 7:9, 12.   “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu    halitanirudia bure bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.   Isa 55:11" Tabia ya mtu mwaminifu. 1. Mtu aliye mwaminifu ni yule ambaye anatenda sawa...