Karibu na endelea kujifunza neno la Mungu katika somo hili linalohusu rafiki wa kweli wa Mungu. Yampasa kila mkristo aliyeokoka kufahamu ya kwamba yeye ni rafiki wa Mungu ikiwa anazingatia maagizo ya neno la Mungu kama ifuatavyo;
1. Kumpenda Mungu na kudumu katika kuzishika amri zake. “ Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nimtapenda na kujidhihirisha kwake”. (Yohana 14:21). “...Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuwa kwake, na kufanya makao kwake. Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; …” (Yohana 14:23,24).
Kutokana na maandiko ya neno la Mungu kama yanavyosema hapa juu, ni lazima mtu awe na upendo wa kweli kwa Mungu kwa kuzishika amri zake. Ikiwa mtu hatazishika amri za Mungu huyo atakuwa hampendi Mungu na wala si rafiki wa kweli wa Mungu. Kwa sababu hiyo mtu huyo hana upendo wa Mungu ukikaa ndani yake.
2. Kudumu katika upendo wa Mungu kwa kuzingatia kuishi sawasawa na neno la Mungu linavyosema. “Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe.” (Yohana 15:10-11). Katika maandiko haya yanaonyesha wazi ya kwamba mtu akikaa (akidumu) katika pendo la Mungu, mtu huyo anakuwa na furaha ambayo Yesu anayo.
3. Kuwa na upendo kamili. Hili ni jambo la muhimu. Mtu nayekuwa na upendo kamili ni mtu ambaye anampenda Mungu na watu wengine. “...Tukipendana, Mungu hukaa ndani yetu, na pendo lake limekamilika ndani yetu”. (1Yohana 4:12). Mtu hawezi kusema anampenda Mungu iwapo atakuwa anamchukia ndugu yake. “Mtu akisema, nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; Kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake”. (1Yohana 4:20-21).
4. Lazima mtu amwamini Mungu na kuishi kwa imani. Tunaweza kujifunza kwa Ibrahim ambaye alikuwa ni rafiki wa Mungu kwa sababu alikuwa anamwamini na kufanya mambo yote ambayo Mungu aliyomwagiza. “Waona kwamba imani ilitenda kazi pamoja na matendo yake, na ya kwamba imani ile ilikamilishwa kwa njia ya matendo yake. Maandiko yale yakatimizwa yalivyonena, Ibrahim alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa ni haki; naye aliitwa rafiki wa Mungu.” (Yakobo 2:22,23).
Kwa sababu hiyo unaweza kuona na kufahamu ya kwamba kuamini na kutenda ni vitu viwili tofauti. Kwanza Ibrahim alimwamini Mungu na pia alitenda sawasawa na Mungu alivyomwagiza. Imani ya namna hii, ndiyo imani iliyokamilika. Haiwezekani mtu kumwamini Mungu peke yake bila kuyatenda aliyoagiza. Mtu afanyaye hivyo hawezi kuwa rafiki wa kweli wa Mungu. Ndio maana imeandikwa; “Mwaona ya kwamba mwanadamu huhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo yake; si kwa imani peke yake”. (Yakobo 2:24).
5. Kuishi kwa imani kwa kumwamini Mungu na kumtegemea katika mambo yote na kufahamu ya kwamba yeye ndiye msaada. Kuishi kwa imani ya namna hiyo ndipo tunampedeza Mungu.
Ijapokuwa mtu atakuwa na mambo magumu au shida yoyote, yampasa kumtegemea na kumtumaini Mungu kwa sababu yeye ndiye msaada katika maisha yetu. Ni muhimu kumtegemea Mungu na kumtumaini kwa sababu kuna mambo mengine kwetu sisi wanadamu hayawezekani, ila kwa Mungu yote yawezekana. Hapa tunaweza kuona anayemtegemea Mungu amebarikiwa na yule asiyemtegemea amelaaniwa. “Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake, Na moyoni mwake amemwacha Mungu...Amebarikiwa mtu yule mtu anayemtegemea Bwana, ambaye Bwana ni tumaini letu”. (Yeremia 17:5,7). “Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, Roho yangu haina furaha naye.” (Waebrania 10:38)
Fuatilia somo lingine hapa kwa kubofya upate kumfahamu,
Maoni
Chapisha Maoni