Ruka hadi kwenye maudhui makuu

KUSUDI LA MUNGU KWA WATUMISHI WAKE.

Hapa tutajifunza na kufahamu kusudi la Mungu kwa watumishi wake aliowachagua au kuwateuwa kwa ajili ya kazi yake. Katika somo hili tutajifunza kusudi kuu ambalo Mungu amewaitia watumishi  wake ambalo ni KUHUBIRI NA KUFUNDISHA neno lake. Hilo ni jambo la msingi kwa ajili ya kuujenga ufalme wa  Mungu. Ni muhimu kuwa makini kuyathibitisha kwanza yale unayotaka kuhubiri au kufundisha, ili usije ukalipotosha kanisa. Yatupasa kufahamu  kwamba wale tunaowafundisha ni watoto wa Mungu waliozaliwa katika  Kristo Yesu wakati walipookoka. Kwa sababu bado ni watoto wachanga hawayajui maandiko ipasavyo hivyo ni rahisi sana kuamini kila kitu wanachofundishwa. Yakupasa mtumishi kujiuliza kuwa J e! yale ambayo nimekua nikihubiri au kufundisha ni sahihi? Kama siyo sahihi yakupasa  kulirekebisha kanisa kwa kulifundisha upya ili  kuliokoa na jehanum ya moto wa milele. Kwa kufanya hivyo utakuwa ni mtumishi mwaminifu. Kumbuka imeandikwa ya kwamba siku ile ya mwisho kila mmoja katika kazi ya utumishi itapimwa mbele za Mungu na kutolewa hukumu.

Ndio maana Mtume Paulo anaonya kwa kusema; “Kwa kadri ya neema ya Mungu niliyopewa, mimi, kama mkuu wa wajenzi mwenye hekima, naliuweka msingi, na mtu mwingine anajenga juu yake. Lakini kila mtu na aangalie jinsi anavyojenga juu yake. Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Kristo Yesu. Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya thamani, au miti au majani au manyasi, kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. Kazi ya mtu aliyeijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu.Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara; ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto.” 1Kor 2:10-15.

Kuna mambo anayotakiwa mtumishi  kuyazingatia  ili aweze kulifahamu zaidi neno la Mungu. Ni haya yafuatayo;  
1.   Kujifunza neno la Mungu kwa bidii kwa kulisoma na kulielewa
2.   Kujifunza kwa kuwasikiliza watumishi wengine wanapofundisha. 
3.   Kujfunza kwa kusoma vitabu vya watumishi wengine.                                                                           
Ni muhimu kwa kila mafundisho ya neno la Mungu kuyachambua na kuyathibitisha na maandiko ili kufahamu ukweli kama ndivyo ulivyo. Kutokujua kanuni hizi ni rahisi kuamini kila kinachofundishwa ambacho mwisho wake ni njia ya upotevu.
Kwa mfano huwezi kutafsiri andiko katika mstari mmoja na kuusimamia peke yake. Ili kupata uthibitisho ni lazima ulinganishe na maandiko mengine katika Biblia. Tunaweza kujifunza kwa wakati ule wa mitume jinsi  watu wa Beroya  walivyokuwa na bidii ya kuyachunguza maandiko. “Mara hao ndungu wakawapeleka Paulo na Sila usiku hata Beroya...Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa  Thesalonike, kwa kuwa walilipokea, lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone mambo hayo ndivyo yalivyo.”  Mdo 17:11.

Ikiwa utajihesabia haki yakwamba unayajua maandiko kuliko wengine na kupuuza kujifunza kutoka kwa wengine, kufanya hivyo ni kujidanganya nafsi yako mwenyewe. Ni jambo la msingi kuendelea kujifunza neno kwa wengine, kwa sababu kila mmoja amepewa ufunuo wa neno la Mungu kwa sehemu, kwa ajili ya kujengana kila mmoja na mwenzake. Ijapokuwa kuna watumishi ambao wamejaliwa kuyafahamu maandiko kwa usahihi na kuyahubiri na kuyafundisha, lakini kuna kitu ambacho watakuwa wamepungukiwa watajifunza kutoka  kwa wengine. Ndio maana imeandikwa; “Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na kufanya unabii kwa sehemu...wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajaua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana.” 1Kor 13:9,12. “Tena pana tofauti za huduma na Bwana ni yeye yule. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa roho kwa kufaidiana (kusaidiana au kujengana) .”1Kor 12:5,7. “Lakini kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadri ya kipimo cha kipawa chake Kristo.” Efe 4:7.
                                                                           Kama ambavyo umeona mwanzoni, nimezungumzia kusudi kuu la Mungu kwa watumishi wake aliowaita kuhubiri na kufundisha neno la Mungu. Je! Watahubiri na kufundisha nini? Fuatana na nami na kuangalia haya yafuatayo; 
1.  Kuwahubiria watu wenye dhambi watubu na kuziacha dhambi zao. Jambo hili tunajifunza kwa Yesu Kristo Bwana wetu na kwa mitume wake.  “Tokea wakati huo Yesu alianza kuhubiri, na kusema, Tubuni, kwa maana ufalme wa Mungu umekaribia.” Mt 4:17. “Tubuni, basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe...” Mdo 3:19.

2.  Kuwafundisha neno la Mungu wale ambao wamekwisha kumwamini Yesu na kuokoka. “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi,...na kuwafundisha kuyashika yote niliyowamuru ninyi...”  Mt 28:18-20.

Kutokana na kusudi kuu ambalo umejifunza ni vyema kuwa na kiasi katika kuhubiri au kufundisha mambo haya yafuatayo;
1. Uponyaji na miujiza. Hapa ninatoa mfano ikiwa mtumishi wa Mungu wakati ameandaa mkutano wa injili kwa kuwatangazia watu kuwa mkutano utafanyika mahali fulani. Siyo sahihi anapowawakaribisha watu ili kusikiliza habari njema na kuwaambia  njoo upokee muujiza wako na wenye shida na magonjwa wataombewa na kuponywa. Lakini jambo la msingi na la kuzingatia ni kuhubiri na kufundisha neno, naye Mungu atajidhihirisha kwa ishara na maajabu kwa ajili ya kulithibitisha neno (fundisho).  Tuangalie mitume wa Yesu kama ilivyoandikwa; “Nao wale wakatoka (mitume) ,wakahubiri kotekote, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo.” Mk 16:20.
  
Ni muhimu kutambua kwamba sisi tu wanadamu hatuna uwezo wa kuponya bali tunapewa uwezo wa kuponya na Mungu mwenyewe. Hapa  ina maana kwamba uwezo wa kuponya si mali yetu na kuutumia kama tupendavyo, bali ni Bwana huwatumia watumishi wake kama apendavyo. Kwa maana hiyo watumishi walioitwa kuifanya kazi ya Bwana wao ni kama chombo ambacho hutumiwa na Bwana.

Ni jambo la kuvunja moyo kwa wale walioamini matangazo ya uponyaji wanapohudhuria kwenye mikutano ya injli wakitarajia kuponywa, lakini baadhi yao ni wachache tu ndio huponywa. Tukiangalia kwa upande wa kanisa neno la uponyaji linafundishwa ni haki ya kila mmoja aliyeokolewa na Bwana anapoliamini neno ataponywa. Ni vyema tukajifunza kwamba Mungu  huponya na kufanya maajabu kwa ajili ya kusudi lake. Ndio maana andiko linasema; “Bwana amefanya kila kitu kwa kusudi lake...” Mit 16:4.  Sehemu nyingine tunamwona Mtume Paulo  sio wote aliwaponya wakati wa utumishi wake. Ndio maana alisema “...Trofimo nalimwacha huko Mileto, hawezi”. 2Tim 4:20b

Yatupasa tujihadhari tusiwahukumu wale ambao hawajaponywa na kudhani ni kwa sababu hawaamini au ni wenye dhambi. Kuna wakati Yesu alikwenda kwenye birika liitwalo Bethzatha ambapo palikuwa na jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza. Ijapokuwa aliwakuta wagojwa wengi kwenye hilo birika, hapo Yesu alimponya mtu mmoja. Soma kwenye Yn 5:1-9. Sehemu nyingine alipokwenda aliwaponya wagonjwa wote. “Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya.” Mt 15:30. Pia unaweza kujifunza wakati Yohana mbatizaji alipokuwa gerezani  Yesu alikuwa anafufua wafu. Lakini Yohana alipouawa Yesu hakumfufua.

Kuna kisa cha mtumishi mmoja na mke wake, mtoto wao aliumwa wakamwombea ijapokuwa hali yake ilizidi kuwa mbaya waliendelea kusimamia imani na kumwamini Mungu kuwa  atamponya, lakini mtoto alikufa. Pia kuna kisa kingine cha mwinjilisti mmoja ambaye Bwana alikuwa anamtumia kuponya wagonjwa. Siku moja alimkuta mtu aliyekuwa mgonjwa alifikiri atakapomwombea Bwana ataponya kama alivyomtumia kuponya wengine, lakini alipomwombea  yule mtu hakuponywa. Kama yule mgonjwa asingewahishwa  hosipitali angekufa.Ikiwa mtu mgonjwa anapoombewa hupona wakati huo huo, kama hajaponywa apelekwe hospitali.

2 .Utajiri au mafanikio.  Hili ni jambo lingine ambalo linahubiriwa au kufundishwa kinyume na neno la Mungu. Ni muhimu kuwa makini kuliangalia neno na kulitumia kupima kila kitu tunachokifanya kama ndivyo kinavyotakiwa.  Neno la Mungu ni kiongozi, linatuongoza kwa kila jambo katika maisha ya hapa duniani.  Vilevile neno la Mungu linatufundisha na kutuweka huru kwa yale tusioyafahamu.  Ndiyo maana imeandikwa; “Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”  Yn 8:32.
Mungu amesema masikini wataendele kuwepo hapa duniani. “Kwa maana masikini hawatakoma katika nchi milele,...” Kum 15:11. 

Kwa hiyo siyo sahihi kuwahubiria watu ya kwamba  Mungu atawafana matajiri ikiwa watamtolea Mungu fungu la kumi, sadaka, au wakitoa michango kwa ajili ya kupeleka injili. Kumtolea Mungu zaka na dhabihu ni sehemu na ni agizo la  kumwabudu kwa kumrudishia utukufu kwa yale aliyokupa au aliyokufanikisha. Kwa kutii na  kufanya hivyo tayari utakuwa umebarikiwa. Kubarikiwa kwa mtu si kwa wingi wa fedha na mali alizonazo pekee, bali ni kwa kuishi sawasawa na neno la Mungu.

Katika maandiko tunajifunza jinsi  Yesu alivyoacha enzi na mamlaka ya  mbinguni, utajiri na uungu aliokuwa nao, akaja duniani kama mtumwa. Kwa sababu hiyo hakuwa tajiri. Naye mama yake Yesu alikuwa ni mtu wa kawaida wala si tajiri. Lakini walikuwa ni wabarikiwa. “Na abarikiwe yeye ajaye kwa jina la Bwana...”  Zab 118:26. “Nayo siku y pili yake watu wengi walioijia sikukuu walisikia Yesu anakuja Yerusalemu...wakatoka nje kwenda kumlaki, wakapiga kelele, Hosana! Ndiye mbarikiwa ajaye kwa jina la Bwana, Mfalme wa Israel.” Yn 12:12-13. “Basi, Mariamu akaondoka siku hizo, akaenda...nyumbani kwa Zakaria akamwamkia Elisabeti. Ikawa Elisabeti aliposikia kuamkia kwake...akajazwa Roho Mtakatifu; akapaza sauti kwa nguvu akasema, umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo lako amebarikiwa.” Lk 1: 39-42.

Injili inayohubiriwa ya mafanikio imewayumbisha watu wengi kwa sababu walitarajia watakuwa na yale yote walioamini na kuombewa. Ni vema tujiulize je! Watu wote waweza kuwa matajiri? Jibu ni hapana kwa sababu Mungu anamngawia kila mtu kipimo au kiasi cha Baraka (mafanikio) “...Kutoa sadaka ya hiari ya mkono wako, utakayoyatoa  kwa kadiri akubarikiavyo Bwana Mungu wako. Kila mtu atoe kwa kadiri  awezavyo, kwa kadiri ya baraka ya Bwana, Mungu wako alivyokupa. ” Kum 16:10,17.

Kutokana na somo hili la utajiri au mafanikio tunaona na kufahamu ya kwamba Mungu anawabarikia watu wake kwa kipimo. Ndiyo maana Mungu amesema kila mtu atoe sadaka kwa kadiri  alivyombariki.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

KUMTUMIKIA MUNGU KWA BIDII.

Kutokana na kichwa cha somo hapa juu katika matukio wazi ili mtu amtumikie Mungu ni lazima awe na bidii. Kwa sababu hiyo kwa mtu yule ambaye ameweka nia moyoni mwake ya kwamba atatumikia Mungu kwa bidii. Tukiangalia kuhusu mwanadamu kuna mambo mengi katika maisha yake ameyafanya kutokana na bidii aliyo nayo. Lakini ikiwa mtu hana bidii kwa ajili ya mambo ya Mungu kamwe hawezi kuingia ufalme wa Mungu. Ndio maana imeandikwa;  "Tangu siku za Yohana Mbatizaji hata sasa ufalme wa mbinguni hupatimkana kwa nguvu, nao wenye nguvu wauteka,   Mathayo 11:12 ."    " Torati na manabii vilikuwapo mpaka Yohana; tangu wakati huo habari njema ya ufalme wa Mungu hutangazwa, na kila mtu hujiingiza kwa nguvu."   Luka 16:16. Hapa ninatoa ushuhuda wangu binafsi, kuhusu kumtumikia Mungu kwa bidii. Wakati nilipookoka nilikuwa na kiu au shauku kwa ajili ya kutaka kujazwa Roho Mtakatifu. Kwa sababu nilikuwa ninamhitaji sana nilimwomba mtumishi mmoja wa Mungu aniombee ili niweze kujazwa...

KUISHI MAISHA YA UTAKATIFU.

Utakatifu  - Ni maisha ya Mkristo anayoyaishi kwa kuzingatia kanuni ya neno la Mungu baada ya kumkiri na kumpokea Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yake. Kuishi maisha ya utakatifu ni jambo linalowezekana, kwa sababu Mungu alipomuumba mwanadamu alimwekea hiari ndani yake kwa kutokea kwa tukio. Ndio maana Yesu alipokuwa akifundisha alitumia mfano wa mti kuonyesha mtu anavyoweza kuishi maisha haya ya kumpendeza Mungu au ya maisha ya dhambi. "   "Ufanye mti kuwa mzuri na matunda yake kuwa mazuri, au ufanye mti kuwa mbaya na matunda yake mabaya, kwa maana kwa matunda yake mti hutambulikana" Mathayo 12:33. Kuishi maisha ya utakatifu ni agizo la Mungu kwa wale wote aliowachagua. Ndio maana Mungu alimwambia Musa,   "Nena na makutano wote na wana wa Israel, uwaambie, mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi Bwana Mungu wenu ni mtakatifu"  Walawi    19:2. Kuwa mtakatifu ni kumpendeza Mungu, kwa sababu amesema;  “Watakatifu waliopo duniani ndio walio bora...

TUNDA LA UAMINIFU.

Uaminifu ni mojawapo ya tunda la Roho katika maandiko matakatifu. Tutajifunza uaminifu wa Mungu unaopatikana katika neno lake. Yeye amesema atatimiza yale aliyoahidi katika neno lake, si tu kwa wana wa Israel bali kwa watu    wote wanaoishi sawasawa na neno lake. Kwa hiyo, kwa upande wetu inatupasa sisi nasi kuwa waaminifu kwa kuliishi na kulitenda neno la Mungu.   “Basi jueni ya kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake, hata vizazi elfu.   Na itakuwa, kwa sababu mwazisikiza hukumu hizi, na kuzishika na kuzitenda, basi Bwana, Mungu wako, atakutimizia agano na rehema aliyowaapia baba zako.”   Kum 7:9, 12.   “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu    halitanirudia bure bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.   Isa 55:11" Tabia ya mtu mwaminifu. 1. Mtu aliye mwaminifu ni yule ambaye anatenda sawa...